Nape awashukia maofisa habari

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amemwagiza Mkurugenzi wa Habari Maelezo kufuatilia utendaji kazi wa maofisa habari na mawasiliano wote ili kuona kama utendaji wao unaleta tija kwa jamii. Nape ametoa kauli hiyo leo (Alhamisi) wakati akizungumza na maofisa habari na mawasiliano kwenye mkutano wao uliofanyika kwenye ukumbi wa hazina ndogo mjini Dodoma. Nape amesema kuna baadhi ya maofisa habari na mawasiliano ambao hawajui majukumu yao na hivyo kukwamisha taarifa mbalimbali ambazo zinatakiwa ziifikie jamii kwa wakati hivyo kusababisha ofisi na taasisi zao kulaumiwa na waandishi wa habari pamoja na jamii inayowazunguka. “Nataka niiagize ofisi ya Mkurugenzi wa habari maelezo kuhakikisha kuwa mnafuatilia utendaji kazi wa kila ofisa habari na mawasiliano ili kujiridhisha kama wanafanya kazi zao kwa mujibu wa sheria au la na kama tutabaini kuna ofisa habari ambaye hatekelezi majukumu yake ipasavyo tumwombe atupishe,” amesema Nape na kuongeza: “Kutoa habari zinazohusiana na taasisi zenu mnazofanyia kazi ni jukumu lenu la kisheria na siyo hiari yenu kwa hiyo hakikisheni kuwa waandishi wa habari wanapowatafuta ili kupata habari kwenye ofisi zenu mnawapa taarifa sahihi na kwa wakati ili jamii iweze kupata majibu ya maswali yao kwa wakati na kwa usahihi.”

Related

kitaifa 4022871585481405619

Post a Comment

emo-but-icon

item
Kicbjamii