Yanga wamkumbuka pluijm.

http://maisharaisi.blogspot.com/2017/03/yanga-wamkumbuka-pluijm.html
Tangu kuenguliwa kwa Hans van der Pluijm kutoka nafasi ya Kocha Mkuu wa Yanga na kuwa Mkurugenzi wa Ufundi na mwishowe kutimuliwa, wapo wapenzi wa timu hiyo walioendelea kumlilia wakiamini Mholanzi huyo ndiye mwarobaini wao. Imani hiyo ilikolezwa na matokeo ya timu hiyo katika baadhi ya mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara, ikiwamo ile dhidi ya watani wao wa jadi, Simba, lakini pia kipute cha Ligi ya Mabingwa Afrika walipoivaa Zanaco ya Zambia mwishoni mwa wiki iliyopita. Katika mechi dhidi ya Simba, Yanga ilijikuta ikikubali kusawazishiwa bao na hatimaye kufungwa la pili na hivyo kulala kwa 2-1, tena ikiwa hivyo wakati wapinzani wao hao wakiwa pungufu ya mchezaji mmoja baada ya Javier Bokungu kutolewa kwa kadi nyekundu mwanzoni mwa kipindi cha pili. Pia, katika mchezo dhidi ya Zanaco, Yanga pamoja na kuanza kufunga bao la kuongoza, ilijikuta ikilazimishwa sare ya bao 1-1 baada ya wapinzani wao hao kusawazisha. Japo wapo wanaoamini matokeo yale yalitokana na hali ya kimchezo tu, lakini baadhi wanadhani iwapo Pluijm angekuwa katika benchi mambo yangekuwa tofauti. Kwa nyakati kadhaa, BINGWA limekuwa likihaha kupata maoni ya Pluijm juu ya imani hiyo ya mashabiki wa Yanga, lakini wakati wote Mholanzi huyo amekuwa akigoma kuzungumza lolote. Lakini baada ya kubanwa jana japo alikataa kata kata kuzungumza lolote juu ya imani waliyonayo baadhi ya watu wa Yanga dhidi yake, alisema neno ambalo linaweza likawa ni ishara njema kwa Wanajangwani wanaomtaka. “Kilio cha mashabiki nimekisikia, lakini kwa sasa sitaweza kuzungumza suala lolote kuhusiana na masuala ya kiufundi wala kilio cha mashabiki juu yangu, nikifanya hivyo nitakuwa ninaharibu utaratibu na ninaweza kuleta mvurugano katika timu, naheshimu maamuzi ya viongozi wa Yanga lakini pia naheshimu kazi anayofanya mwalimu wa sasa, muda ukifika kila kitu kitakuwa wazi,” alisema Pluijm. Lakini pamoja na mtaalamu huyo kutoa kauli hiyo, BINGWA linafahamu kuwa kigogo mmoja wa Serikali ambaye amekuwa karibu mno na Yanga, yupo katika mikakati ya kuhakikisha Pluijm anarejeshwa katika majukumu yake ya awali. Kigogo huyo ambeya ameshawahi kufanya jitihada kede kede kuisaidia Yanga pale ilipobidi, aliwashukia wajumbe wa Kamati ya Mashindano ya klabu hiyo kwa kufanya maamuzi kadha wa kadha ambayo mwisho wa siku yaliigharimu klabu, ikiwamo kung’olewa kwa Pluijm. Mmoja wa watu wa ndani ya Yanga, alisema kuwa kigogo huyo aliwachana wajumbe hao kwa kuwaita vigeugeu kwani hata baada ya ujio wa mrithi wa Pluijm, George Lwandamina, wameonekana kumgeuka na kumkosoa hadharani Mzambia huyo, hasa katika suala zima la kufanya mabadiliko ya wachezaji. Pamoja na yote hayo, Yanga bado inaonekana kuwa katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wake wa Bara, lakini pia kufanya vema kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, iwapo mashabiki, wanachama, wachezaji na viongozi wa klabu hiyo nchi nzima watajipanga upya na kupiga hesabu zao ipasavyo. Katika hatua nyingine, kikosi cha Yanga kinatarajiwa kuondoka nchini Alhamisi kwa ndege ya Shirika la Kenya Airways kwenda Zambia tayari kuivaa Zanaco, kwa mujibu wa habari zilizopatikana jana jioni.